Tunahitaji tafiti bora za mbegu – Bashe

Naibu Waziri wa Wizara ya Kilimo Hussein Bashe jana (10/10/2019 ) aemeshauri Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine na Wakala wa Uzalishaji Mbegu Tanzania (ASA) kushirikiana kuzalisha mbegu bora ili kukidhi mahitaji ya wakulima.
Amesema taasisi za Serikali zinapasa kuwa mdau wa kwanza katika kuhakikisha mbegu bora na za kutosha zinapatikana.
“Usalama wa Chakula utakuwa endelevu endapo hatua madhubuti zitachukuliwa kuona taifa linazalisha mbegu za kutosha na zinazohimili magonjwa” alisema Naibu Waziri


Bashe yupo mkoani Morogoro kwa ziara ya kikazi kukagua shughuli za uzalishaji mbegu ambapo alifanya mikutano na wakuu wa Viongozi wa Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine,Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI) pamoja na Wakala wa Mbegu (ASA)
Bashe alisitiza kuwa uchumi hauwezi kukua kama hakutakuwa na uwekezaji mzuri kwenye kilimo kwa kutumia utaalam unaopatikana kwenye taasisi za kitaaluma.
Naibu Waziri alibainisha kuwa ni lazima kilimo kiangaliwe kwa jicho la kibiashara ili kiweze kumvutia mkulima na wawekezaji hivyo ni wakati wa wataalamu wa kilimo kuchochea mabadiliko chanya.
“Ni muda muafaka sasa tafiti nyingi za SUA zitokane na matatizo ya wakulima ili waweze kuzitumia na kubadilisha kilimo chao kuwa chenye tija” alisema Bashe
Naye Makamu Mkuu wa Chuo Prof Raphael Tihelwa Chibunda amesema chuo chake kipo tayari kufuata maelekezo kwa kuwa tafiti zao zote zinalenga mahitaji ya jamii ya watanzania.
Prof Chibunda amesema pamoja na kuongeza uzalishaji wa mbegu lakini ni muhimu kama nchi kuimarisha huduma za ugani ili kuleta matokeo mazuri pindi wakulima watakapotumia mbegu bora za kilimo
Hata hivyo amemweleza Naibu Waziri kwamba imefika wakati nchi kuondokana na kuweka vikwazo zadili (regulatory) badala yake iwe na mikakati ya promosheni kwa kuwa bado hatujawa na utoshelevu katika mbegu.

Share your views about this story

Related stories

Subscribe to Kilimo News

Get the latest agriculture news in East Africa